1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Usafi ndiyo adui wa Kipindupindu

30 Mei 2019

Kipindupindu ni ugonjwa hatari unaosababishwa na bakteria aitwaye "vibriocholerae" na huathiri hasa utumbo mwembamba. Bakteria hao husababisha kuhara na kutapika sana pamoja na homa kali.

https://p.dw.com/p/3JUuP
Bakterien Erreger der Cholera
Picha: picture-alliance/Dr.Gary Gaugler/OKAPIA

Kwa kawaida hupatikana katika chakula au maji machafu na kinyesi kutoka mtu aliye na maambukizi. Kwa hiyo, huambukizwa kwa njia zifuatazo:

·   Usambazaji wa maji machafu

·   Barafu iliyotengenezwa kwa maji machafu

·   Vyakula na vinywaji vilivyo na bakteria

·   Mboga zilizopandwa kwenye maji taka

·   Samaki na dagaa waliovuliwa kwenye maji machafu

Makundi yanayoweza kuambukizwa kwa haraka:

1.  Wasafiri

2.  Sehemu zenye mikusanyiko ya watu wanaokula kama hotelini, harusini na kadhalika.

3.  Wafanyakazi wa afya

4.  Waandaji wa vyakula mtaani (Mama ntilie).

5.  Wakazi wa makazi duni

6.  Wavuvi

7.  Watoto

Dalili za kipindupindu

Mosambik Cholera Idai Zyklon
Picha: Getty Images/W. De Wet

Dalili za ugonjwa wa kipindupindu zinaweza kuonekana ndani ya masaa machache au siku tano baada ya maumbukizi.

Dalili hizo ni:

·   Kuharisha maji maji (maji yanayofanana na maji ya mchele)

·   Kutapika

·   Mapigo ya moyo kwenda haraka

·   Upungufu wa maji mwilini unaosababisha kusinyaa kwa ngozi, ukavu wa mdomo, koo, na pua

·   Kushuka kwa shinikizo la damu

·   Maumivu ya misuli

·   Kiu mara kwa mara

Maambukizi ya kipindupindu ni kawaida kwa makazi ya mijini na vijijini au katika mazingira yenye upungufu wa maji safi.

Jinsi ya kuzuia ugonjwa wa Kipindupindu

Njia zifuatazo husaidia kuzuia ugonjwa wa kipindupindu:

·   Kuzingatia njia sahihi za usafi.

·   Kunawa mikono kwa sabuni mara kwa mara, hasa baada ya kutumia choo na kabla ya kushika chakula.

·   Matumizi ya vyoo wakati wote.

Symbolbild Nigeria Cholera
Picha: picture-alliance/dpa/Gilbertson

·   Tumia maji safi na salama yaliyo chemshwa, ama yaliyo changanywa na kemikali ya kuua wadudu, au maji ya chupa kwa matumizi yafuatayo:

- Kunywa

- Kuandaa chakula au vinywaji

- Kutengeneza barafu

- Kusafisha meno

- Kuosha uso wako na mikono

- Kuosha vyombo

- Kuosha matunda na mboga

Usitumie / usile chakula kibichi, kama vile:

·   Matunda na mboga ambazo hazijamenywa

·   Maziwa ambayo haijachemshwa

·   Nyama na Samaki ambao hawajapikwa