1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIran

UNRWA ina mifumo ya kuhakikisha haiegemei upande wowote

Tatu Karema
22 Aprili 2024

Tathmini mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuwahudumia Wakimbizi wa Palestina, UNRWA, imegundua kuwa shirika hilo lina mifumo thabiti ya kuhakikisha uzingatiaji wa sera zisizoegemea upande wowote

https://p.dw.com/p/4f3xp
Lori lililobeba bidhaa za msaada kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA) likingoja kwenye foleni kuingia katika maeneo ya Palestina kutoka kwenye kivuko cha mpaka cha Rafah mnamo Novemba 19,2023.
Lori lililobeba bidhaa za msaada la shirika la UNRWAPicha: Gehad Hamdy/dpa/picture alliance

Nakala ya tathmini hiyo iliyoonekana na shirika la habari la Reuters, imesema kwamba ripoti hiyo ambayo inaweza kuwafanya baadhi ya wafadhili kuzingatia upya ufadhili wao kwa shirika hilo, pia imebainisha kuwaIsrael bado haijatoa ushahidi wa madai yake kwamba idadi kubwa ya wafanyakazi wa UNRWA walikuwa wanachama wa makundi ya kigaidi.

Waziri wa zamani wa ufaransa aliongoza jopo la tathmini

Umoja wa Mataifa ulimchagua waziri wa zamani wa Ufaransa, Catherine Colonna, kuongoza jopo hilo la kufanya tathmini ya kutoegemea upande wowote shirika hilo la UNRWA mnamo mwezi Februari, baada yaIsraelkudai kwamba wafanyakazi 12 wa shirika hilo walihusika katika shambulizi la kushtukiza la Hamas dhidi ya Israel la Oktoba 7, lililochochea vita katika Ukanda wa Gaza.

Soma pia:Japan kuanza tena kulifadhili shirika la UNRWA

Ripoti ya mwisho ya jopo hilo linaloongozwa na Colonna, inatarajiwa kutolewa rasmi baadaye leo.

Katika uchunguzi tofauti, chombo kimoja cha uangalizi cha Umoja wa Mataifa, pia kinachunguza madai hayo dhidi ya wafanyakazi wa UNRWA.

Iran yasema itajibu ikiwa kutakuwa na shambulizi lingine kutoka Israel

Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Iran, Nasser Kanaani, amesema leo kwamba lile lililotajwa kuwa shambulizi la anga la Israel karibu na kituo kimoja kikubwa cha wanajeshi na kiwanda cha nyuklia katikati mwa Iran, ni tukio la ''uchokozi'' ambalo halikusababisha uharibifu wowote.

Rais wa Iran Ebrahim Raisi akzungumza wakati wa mkutano wa serikali mjini Tehran mnamo Novemba 1, 2023
Rais wa Iran Ebrahim RaisiPicha: Iranian Presidency via ZUMA Press/picture alliance

Kanaani ameongeza kuwa iwapo kitendo kingine cha uchokozi kitafanywa kutoka popote pale, au ikiwa mtu yeyote atausaidia utawala wa Kizayuni kufanya uchokozi mwingine, Iranitatoa jibu thabiti na lenye nguvu zaidi.

Kanaani ameongeza kuwa kwa maoni yao, suala hilo halistahili kujadiliwa.

Soma pia:Iran yaashiria haina mpango wa kujibu shambulizi la Israel

Siku ya Ijumaa, mataifa hayo mawili yalipuuza shambulizi hilo la Israel na kuashiria kuwa mataifa hayo hasimu yako tayari kuepeusha mzozo huo kutanuka zaidi katika kanda hiyo.

Miili zaidi yapatikana Khan Younis 

Mjini Khan Younis, miili zaidi imepatikana katika kile ambacho mamlaka ya Palestina imekitaja kuwa makaburi ya halaiki katika eneo la hospitali lililoachwa na wanajeshi wa Israel.

Soma pia:Miili 73 zaidi yafukuliwa katika kaburi la pamoja la Khan Younis

Ahmed Rezik, mwenye umri wa miaka 42 aliyepata hifadhi katika shule moja magharibi mwa Khan Younis, ameliambia shirika la habari la Reuters kwamba familia nyingi zilikuwa zimeondoka eneo hilo wiki mbili zilizopita kurudi kwao mjini Abassan, lakini sasa zimerejea tena.

Rezik anasema watu hao walionekana kuwa na uoga mwingi.