1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi Marekni: Urusi haimtaki Biden, China yampinga Trump

Iddi Ssessanga
13 Agosti 2020

Maafisa wa ujasusi nchini Marekani wanaamini Urusi inaendesha njama dhidi ya mgombea wa chama cha Democratic Joe Biden, huku washirika wa Kremlin wakifanyakazi kuimarisha kampeni ya Trump.

https://p.dw.com/p/3guwz
Bildkombo Donald Trump und Joe Biden

Mkuu wa kitengo cha kupambana na ujasusi wa nje nchini Marekani, amesema maafisa wa ujasusi nchini humo wanaamini kuwa Urusi inatumia njia mbalimbali kumpaka matope mgombea urais wa chama cha Democratic Joe Biden, kuelekea uchaguzi mkuu wa mwezi Novemba, na kwamba watu wenye mahusiano na ikulu ya Kremlin wanafanya juhudi za kuipa nguvu kampeni ya kuchaguliwa tena kwa rais Donald Trump.

Katika onyo makhsusi zaidi kuhusu kitisho cha uingiliaji wa kigeni kwenye uchaguzi wa Marekani, mkuu huyo wa kitengo cha kukabiliana na ujasusi wa nje William Evanina, alisema maafisa wa ujasusi wanaamini pia kwamba China haitaki Trump ashinde muhula wa pili na imeongeza ukosoaji wake wa ikulu wa White House, ikipanua juhudi zake za kushawishi sera ya umma nchini Marekani, ili kuwawekea shinikizo wanasiasa wanaoonekana kuwa wapinzani wa maslahi ya China.

Taarifa hiyo ya Evanina inaaminika kuwa tangazo la wazi kabisaa kutoka kwa jumuiya ya ujasusi ya Marekani, kuhusisha juhudi za ikulu ya Kremlin kumsaidia Trump achaguliwe tena - mada nyeti kwa rais ambaye amekuwa akikataa tathmini za mashirika ya ujasusi kwamba Urusi ilijaribu kumsaidia mwaka 2016.

Inaunganisha pia upinzani wa Moscow dhidi ya Biden, kwa nafasi yake kama makamu wa rais katika kuunda sera za utawala wa Obama katik kuisaidia Ukraine, ambayo ni mshirika muhimu wa Marekani, na kumpinga kiongozi wa Urusi Vladmir Putin.

Trump asema amekuwa mkali kwa Urusi kuliko rais yeyote

Democrats wazissisimua upya siasa za Marekani

Alipoulizwa kuhusu tathimini hiyo ya idara ya ujasusi Ijumaa mjini Bedminster, New Jersey, Trump alionekana kupinga wazo kwamba Urusi inamshushia hadhi Biden. Lakini alionekana kukubaliana na taarifa zinazoonyesha kwamba China haitaki ashinde.

"Nadhani mtu wa mwisho ambaye Urusi ingependa kumuona madarakani ni Donald Trump, kwa sababu hakuna mtu amekuwa mkali kwa Urusi kuliko mimi. Angalia tulivyofanya na jeshi letu, angalia tulivyofanya katika kuweka wazi suala la bomba ambapo mabilioni yanakwenda Urusi. Angalia mambo yote tuliyoyafanya na NATO."

"Tumeingiza dola bilioni 130 kutoka mataifa yaliokuwa hayatimizi wajibu wao na kiasi hicho kitafikia dola bilioni 400 katika miaka michache ijayo, na hiyo yote ni pesa ya ulinzi dhidi ya Urusi. Na China ingependa kumuona Joe Biden akishinda kwa sababu Joe Biden akiwa rais, Chinai tamiliki nchi yetu," alisema Trump.

Soma pia Hata Rais wa Marekani Donald Trump hayuko juu ya sheria.

Taarifa hiyo ya Evanina, ikiwa imesalia miezi mitatu kabla ya uchaguzi, inakuja katikti mwa ukosoaji kutok kwa spika wa baraza la wawakilishi la bunge Nancy Pelosi na wabunge wengine wa Democratic, kwamba mashirika ya ujasusi yamekuwa yakiuficha umma taarifa makhsusi kuhusu kitosho cha uingiliaji wa kigeni katika siasa za Marekani.

USA russiche Wahlinterferenz in Facebook
Baadhi ya matangazo ya Facebook yanayohusishwa na juhudi za Urusi kuvurug mchakato wa uchaguzi wa Marekani na kuchochea mtafaruku miongoni mwa raia wa Marekani.Picha: picture-alliance/AP Photo/J. Elswick

Washirika wa Krelimlin wamfanyia ushawishi Urusi

Mbali na Urusi na China, ripoti hiyo pia inaitaja Iran, na kuonya kuwa maadui wa nje wanaweza kutaka kuhatarisha miundombinu ya uchaguzi, kuingilia mchakato wa kupigakura au kuyafanya matokeo ya uchaguzi yatiliwe mashaka. Licha ya juhudi hizo, mafisa wanaona kama jambo lisilowezekana kwamba mtu yeyote anaweza kuchezea matokeo ya kura katika njia yoyote kubwa, alisema Evanina.

Wasiwasi kuhusu uingiliaji kwenye uchaguzi unazidi hasa kufuatia juhudi kubwa zilizofanywa na Urusi kuingilia uchaguzi wa mwaka 2016 kwa niaba ya Trump kupitia udukuzi wa mfumo wa barua-pepe wa chama cha Democratic na kampeni ya siri ya mitandao ya kijamii iliyolenga kusababisha mtafaruku miongoni mwa wapigakura wa Marekani.

Soma pia Maoni: Trump aongeza joto kwa kupendekeza kusogeza uchaguzi

Trump mara zote amepinga madai kwamba Kremlin ilimpendelea mwaka 2016, lakini tathmini ya mashirika ya ujasusi iliyotolewa Ijumaa iliyopita inaonyesha kuwa watu wenye mafungamano na Kremlin ambao hawakutajwa majina, wanafanya kazi kuimarisha kampeni yake kwenye mitandao ya kijamii na televisheni nchini Urusi.

Chanzo: AP