1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rwanda yakanusha madai ya Kongo dhidi ya kampuni ya Apple

Tatu Karema
27 Aprili 2024

Mamlaka nchini Rwanda imeishtumu serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa kile ilichokitaja kuwa madai yasiokuwa na msingi dhidi ya kampuni ya teknolojia ya mawasiliano ya Apple.

https://p.dw.com/p/4fFbd
Nembo ya kampuni ya Apple
Nembo ya kampuni ya ApplePicha: CFOTO/NurPhoto/IMAGO

Matamshi ya Rwanda yametolewa baada ya Kongo kuishtumu kampuni hiyo kwa kutumia kwenye bidhaa zake, madini yanayosafirishwa kinyume cha sheria kutoka nchini humo.

Hapo jana Ijumaa, msemaji wa serikali ya Rwanda Yolande Makolo, aliliambia shirika la habari la AFP kwamba hii ni hatua ya hivi karibuni zaidi ya serikali ya Kongo ambayo inajaribu kwa mara nyingine kuiangazia Rwanda kwa shtuma za uongo.

Soma pia: Umoja wa Mataifa waonya kuhusu kuendelea kuzorota kwa hali ya usalama Mashariki mwa Kongo

Siku ya Alhamisi, mawakili wa Kongo waliishtumu kampuni ya Apple kwa kununua madini yaliochimbwa kutoka mashariki mwa nchi hiyo na kuingizwa nchini Rwanda kinyume cha sheria, ambapo baadaye husafishwa na kuingizwa katika soko la kimataifa.

Mawakili hao waliwasilisha notisi rasmi kwa Apple ya kuionya kwamba huenda ikakabiliwa na hatua za kisheria ikiwa itaendelea kununua madini hayo.