1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiIsrael

Palestina yahofia maisha ya walionasa hospitali ya Al-Shifa

Bruce Amani
16 Novemba 2023

Maafisa wa matibabu wa Kipalestina wameelezea hofu kuhusu maisha ya mamia ya wagonjwa na madaktari katika hospitali kubwa kabisa ya Gaza, ambao wamenasa baada ya vikosi vya Israel kuivamia.

https://p.dw.com/p/4YtEB
Hospitali ya Al-Shifa huko Ukanda wa Gaza
Maelfu ya wagonjwa, wafanyakazi na raia wanaokimbia mapigano wamekwama kwenye hospitali ya Al-shifa Picha: Khader Al Zanoun/AFP

Wizara ya Afya ya Gaza imesema wanajeshi wa Israel wameondoa miili kutoka hospitali ya Al-Shifa na kuharibu maeneo ya kuegesha magari lakini hawaruhusu wahudumu au wagonjwa kuondoka.

Msemaji wa wizara hiyo amesema hakuna maji, chakula wala maziwa ya watoto, kwenye hospitali hiyo yenye wagonjwa 650 na karibu watu 7,000 waliohifadhiwa kutokana na mashambulizi ya Israel ya angani na ardhini kwa wiki kadhaa.

Kwingineko, Israel imewaamuru leo raia kuondoka kwenye miji minne ya kusini mwa Ukanda wa Gaza, hatua inayoongeza hofu kuwa vita hivyo vinaweza kusambaa hadi maeneo ambayo iliwaambia watu wangekuwa salama.