1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSaudi Arabia

Je, Mwanamfalme wa Saudia ananyoosha mkono wa amani?

Admin.WagnerD3 Aprili 2023

Tangu Mwanamfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman ameingia madarakani, imekuwa vigumu kupata mzozo katika Mashariki ya Kati ambao haumuhusishi kwa njia fulani mrithi huyo wa kiti cha enzi mwenye umri wa miaka 37.

https://p.dw.com/p/4Pe1L
DW Middle East - Saudi Arabia: National makeover in full swing
Mwanamfalme wa Saudi Arabia, Mohammed bin SalmanPicha: ATHIT PERAWONGMETHA/AFP/Getty Images

Sasa anaelekea kwenye mpango wa ujasiri wa kuipa amani nafasi. 

Hatua za kufikia makubaliano na Iran, kuanzisha upya uhusiano na Syria na kumaliza vita vya miaka mingi vya ufalme huko Yemen vinaweza kumuondoa Mwanamfalme Mohammed kutoka kwa baadhi ya masuala ya kikanda ambayo ni miiba anayokabiliana nayo.

Ikiwa atafaulu itakuwa na athari kubwa kwa Mashariki ya Kati juu ya mipango yake ya kuunda upya ufalme wake mbali na masuala ya mafuta lakini zaidi katika sera yake. Kushindwa kwake kunatishia sio tu ujio wake wa kutawala taifa muhimu kwa usambazaji wa nishati duniani, lakini zaidi eneo linaotikiswa na miaka mingi ya mivutano, ambayo kwa sehemu yamesababishwa na maamuzi yake.

Mwamko wa Mwanamfalme Mohammed uliongezeka mnamo 2015 baada ya babake, Mfalme Salman, kumteua kama naibu mkuu wa taji la Ufalme.

Mwaka huo pia mwanamfalme Muhammad alihudumu pia kama waziri wa ulinzi wa nchi hiyo, na aliitumbukiza Saudi Arabia katika kampeni ya kijeshi nchini Yemen, vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vilibadilika na kuwa vita vya wakala wa kikanda na bado vinaendelea hadi leo.

Riyadh inaiunga mkono serikali ya Yemen iliyoko uhamishoni dhidi ya waasi wa Houthi wanaoungwa mkono na Iran ambao wanaushikilia mji mkuu Sanaa.

Kumekuwa pia na mvutano kati ya Saudia na Iran

Jemen | Kämpfer gegen die Huthi-Rebellen nahe Marib
Picha: Nariman El-Mofty/AP Photo/picture alliance

Mvutano na Iran, wakati huo bado katika makubaliano ya nyuklia na mataifa yenye nguvu duniani, uliongezeka baada ya Saudia kumyonga muhubiri wa Kishia mashuhuri mwaka wa 2016. Waandamanaji walivamia ofisi za kidiplomasia za Saudia huko Iran na Riyadh ilivunja uhusiano na Tehran.

Mnamo 2017, Saudi Arabia iliungana na mataifa mengine matatu ya Kiarabu kuisusia Qatar, ambayo inadumisha uhusiano na Iran. Mwaka huo huo, mwanamfalme Mohammed alifanya kile kilichoonekana kama jaribio kubwa la kuvunja uungwaji mkono wa Iran utawala wa Hezbollah kwa serikali ya Lebanon kwa kumualika waziri mkuu wa Lebanon na kisha kudaiwa kumlazimisha kutangaza kujiuzulu. Jaribio hilo halikufanikiwa na ushawishi wa Saudi Arabia nchini Lebanon ulipungua tangu wakati huo.

Siku chache baadaye, mwanamfalme Mohammed alizindua mpango unaodaiwa kuwa dhidi ya ufisadi, kampeni ambayo ilisababisha wasomi wa Saudi kufungwa hadi walipokabidhi mabilioni ya mali. Pia kuuawa kwa mwandishi wa habari Jamal Khashoggi katika ubalozi mdogo wa Saudia mjini Istanbul, ambapo inaaminika na Marekani na wengine kwamba ni kufuatia amri ya mwanamfalme huyo.

Liko pia nafasi ya ushirikiano kati ya Saudia na Urusi kupitia OPEC+

Organization of the Petroleum Exporting Countries (OPEC)
Picha: RYAD KRAMDI/AFP/Getty Images

Wakati huo huo, Saudi Arabia ilidumisha uhusiano wa karibu na Urusi kama sehemu ya nchi zinazosafirisha mafuta kwa wingi duniani (OPEC+), licha ya kuongezeka kwa bei ya nishati kutokana na uvamizi wa Moscow nchini Ukraine na kuibua hasira kutoka kwa Rais Joe Biden na wabunge wa Marekani.

Urusi na China zinatoa nafasi kwa Saudi Arabia na Mwanamfalme Mohammed kuheshimiwa na mataifa makubwa duniani bila ya ukiukaji wa masuala ya haki za binadamu yanayoendelea katika nchi za Magharibi.

Mkataba wa upatanishi wa China kuhusu ufalme huo kuanzisha tena uhusiano na Iran pia unampa Mwanamfalme Mohammed fursa mpya ya kuionyesha Marekani kwamba nchi nyengine zinaweza kuunda siasa za Mashariki ya Kati.

Vikwazo vya Marekani dhidi ya Tehran kuhusu mkataba wa nyuklia ulioporomoka na bado unayumbisha uchumi wa Iran. Kwa Mwanamfalme Mohammed, ameonekana kuitumia fursa kurekebisha uhusiano wake na Iran.

Tayari, Saudi Arabia iliongoza juhudi za kurejesha uhusiano na Qatar mwaka 2021. Kupunguza mvutano na Iran kunaweza kumpatia njia ya kufanya hivyo hatimaye kujiondoa kikamilifu katika vita vya Yemen.