1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uingereza na Zimbabwe

Ramadhan Ali 6 Desemba 2007

Kuhudhuria rais Mugabe mkutano wa kilele kati ya Umoja wa Ulaya na Umoja wa Afrika Lisbon kunatatanisha mkutano.

https://p.dw.com/p/CYJ8
Rais Mugabe wa ZimbabwePicha: AP

Waziri mkuu Gordon Brown wa Uingereza amegoma kuhudhuria mkutano wa kilele unaoanza jumamosi hii mjini Lisbon ,Ureno kati ya Umoja wa Ulya na Afrika.Waziri mkuu wa Zambia Levy Mwanawasa akimuungamkono rais Mugabe alisema ingelikuwa bora kwa waziri mkuu Brown kuhudhuria na kuleta kesi yake mkutanoni.

Kanzela Angela Merkel wa Ujerumani,akitembelewa mjini Berlin na rais Mwanawasa,amesema anauheshimu uamuzi wa waziri mkuu Brown ,lakini anahisi uhusiano baina ya ulaya na Afrika jinsi ulivyo muhimu wakati huu,hangependelea kuona kisa cha nchi moja kinagubika kivuli chake juu ya mkutano wa Lisbon.

Swali la kuhudhuria kwa waziri mkuu wa Uingereza au rais mugabe wa Zimbabwe kikao hiki cha jumamosi mjini Lisbon,Ureno ni mzozo mpya ulioibuka kati ya nchi hizi mbili-Uingereza na Zimbabwe.Ni kisa ambacho wachambuzi wa kisiasa wanaona Mugabe aweza kukitumia kufufua mashtaka yake ya ukoloni mambo-leo wa uingereza na nchi za magharibi dhidi ya nchi yake.Usuhuba kati ya London na Harare haukua daima hivyo.Kulikua na nyakati za maskizano.

Uingereza ilisimamia na kuongoza mazungumzo ya Lancaster House hapo 1979 yalioiongoza iliokua Rhodesia katika uhuru hapo April, 1980 na kumuona Mugabe anaparamia ngazi ya madaraka –kwanza kama waziri mkuu na baadae kama rais.

Mahusiano kwa jumla yalikuwa mema katika kipindi takriban kizima cha 1980 na hata 1990 licha ya tofauti za hapa na pale juu ya msimamo kuhusu Afrika kusini chini ya utawala wa wazungu na sera yao ya ubaguzi na mtengano-aparthied.Lakini, pale waziri mkuu aliepita Tony Blaier kuja madarakani ufa ukaanza kuingia katika usuhuba huu.

Wakati wa mkutano wa Jumuiya ya madola huko Edinburgh,Scotland, 1979, Mugabe alilizusha swali la ahadi aliotoa mtangulizi wa Blair,Johan Major la kuuendeleza mradi wa kununua ardhi za wazungu kuwafidia waafrika.Kwani, ardhi ndio iliokua mzizi wa fitina uliosababisha vita vya ukombozi dhidi ya serikali ya Smith iliojitangazia uhuru,1965.

Kati ya 1980 na 1997, alipoingia Blair madarakani, Uingereza kwa kweli, ilichangia ununuzi wa ardhi za wazungu ili kuwafidia waafrika kwa kima cha pauni milioni 44.

Jibu la Blair halikumpendeza Mugabe na hata msimamo aliouchukua huko Scotland.Changamoto ikiaanza na kutuhumiana hadi leo.

Wachambuzi wanahisi kubadili nia kwa serikali ya uingereza na kuibuka kwa chama chenye nguvu cha upinzani nchini Zimbabwe dhidi ya Mugabe, kulimpalilia Mugabe kusonga mbele kunyakua ardhi za wakulima wa kizungu hapo 1999.Hii ikazusha malalamiko kutoka London na nchi nyengine za magharibi washirika wa Uingereza.

Kwa jicho hili, uangaliwe mvutano huu na wingu lililofunika mkutano huu wa Lisbon kati ya Umoja wa Ulaya na Afrika na kitisho cha Gordon Brown kuususia iwapo Mugabe atahudhuria.Na Mugabe amesema anakwenda Lisbon.

Rais Levy Mwanawasa wa Zambia,akiwa ziarani nhini Ujerumani alisikitishwa mjini Berlin na uamuzi wa Gordon Brown wa kususia kikao cha Lisbon.Amedai kuwa hakuna kitachopatkkana kwa kususia mkutano kwa kuwa tu Mugabe anahudhuria.

Nae Kanzela Angela Merkel wa Ujerumani, mwenyeji wake, wakati akiuheshimu uamuzi wa waziri mkuu wa Uingereza, alisema:

“Tunaheshimu uamuzi wa waziri mkuu wa uingereza.Lakini nikizungumza kwa niaba ya Ujerumani, ninahisi kuwas uhusiano baina ya ulaya na Afrika jinsi ulivyo muhimu kwetu sisi ,tusingependa kuona mazungumzo yetu yamechafuliwa na kisa cha nchi moja-Zimbabwe.”

Kanzela Merkel alisema kuwa, Afrika na Ulaya ni majirani na wanabidi kuzungumzia maswali tangu ya kisiasa hata ya kiuchumi yenye kuzihusu pande hizo mbili.Akaahidi kulizungumzia pia swali la uvunjaji wa haki za binadamu katika mkutano huo wa Lisbon na sitaona haya kutoa maoni yangu juu ya visa vinavyopita Zimbabwe-aliahidi Kanzela Merkel.

Kuhusu maendeleo ya nchi yake, rais Levy Mwanawasa alikumbusha:

“Mnamo miaka ya 1990,Zambia imefanya mabadiliko makubwa ya kuufufua uchumi wake kuelekea soko huru.Nafasi nyingi za kazi zikapotea katika kufanya hivyo kwavile ukuaji wa uchumi ndio kwanza sasa unaanza…”

Rais wa Zambia,alietishia binafsi kuugomea mkutano wa Lisbon ikiwa rais Mugabe atasusiwa kuhudhuria.Kwa kila hali, rais Mugabe na Zimbabwe,hazitaepuka kuwa mada ya mkutano wa Lisbon kati ya Ulaya na Afrika.